Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

DKT.BITEKO ALITAKA SHIRIKA LA...

DKT.BITEKO ALITAKA SHIRIKA LA MAENDELEO YA PETROLI KUONGEZA KASI YA UENDELEZAJI VITALU VYA MAFUTA NA GESI ASILIA

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ameliagiza Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuongeza kasi ya uendelezaji wa Vitalu vya utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia ikiwemo Mnazi Bay Kaskazini, Eyasi Wembere, Songo Songo Magharibi na Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia (LNG) ili nchi iendelee kuwa na uhakika wa upatikanaji wa nishati kwa ajili ya soko la ndani na nje.

Ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akizindua Mkakati wa Muda Mrefu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wa miaka 25 (2024/25 hadi 2049/50) ambao umeweka mipango na malengo makubwa ya kuleta uhakika wa upatikanaji wa nishati nchini, mkakati ambao utaisaidia nchi kutumia kikamilifu rasilimali za mafuta na gesi zilizopo katika maeneo mbalimbali.

”Tunapozindua Mpango Mkakati huu wa miaka 25, ni muhimu tutambue kuwa jukumu muhimu la TPDC ni kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa nishati nchini. Ni muhimu sisi sote hapa tukumbuke kuwa Sekta ndogo ya Mafuta na gesi ina mchango mkubwa sana katika maendeleo ya Taifa hili.” Amesema Dkt. Biteko

Aidha, Dkt. Biteko ameiagiza TPDC kuimarisha mtandao wa mabomba na mifumo ya usambazaji wa gesi nchini ikiwemo kupitia teknolojia za Mini-LNG na CNG ili kuwafikia wananchi wengi ambao wapo mbali na Bomba la Usafirishaji wa Gesi Asilia kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam ili kusaidia kuwafikishia watanzania manufaa yatokanayo na matumizi ya gesi asilia.