Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

KAMATI YA BUNGE YAPONGEZA KASI...

KAMATI YA BUNGE YAPONGEZA KASI YA UJENZI KITUO CHA KUPOZA UMEME CHALINZE

Mradi wafikia asilimia 93.7

Ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka JNHPP wafikia 99.5%

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeeleza kuridhishwa kwake na kasi ya ujenzi wa mradi wa kituo cha kupoza umeme cha Chalinze unaojumuisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka JNHPP hadi Chalinze.

Hayo yalisemwa Mei 18, 2024 na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Kirumbe Ng’enda kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Mathayo David Mathayo wakati wa ziara ya kutembelea mradi huo unaosafirisha umeme unaozalishwa kutoka Bwawa la Julius Nyerere-(JNHPP) hadi kituo cha kupoza umeme cha Chalinze.

"Tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kuendelea kutekeleza miradi ya nishati, kasi ya ujenzi wa mradi huu imeongezeka kutoka asilimia 55 ya mwaka jana na kufikia asilimia 93.7 mwaka huu‘.’ Alisisitiza Mhe. Kirumbe

Alisema Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imefanya kazi kubwa katika kutekeleza mradi huo ambapo ujenzi wa jengo la mitambo umekamilika kwa asilimia 100.

Ameeleza kuwa kukamilika kwa utekelezaji wa mradi huo utazidi kuimarisha hali upatikanaji wa umeme wa nchini na mwingine kuuzwa nje ya nchi pale mahitaji yanapotosheleza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga akizungumza kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko aliwashukuru Wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge kwa ufuatiliaji na ukaguzi wa mradi huo ambao una maslahi mapana kwa Taifa zima na kuahidi kuendelea kuyafanyia kazi maelekezo yanayotolewa na wajumbe hao.

"Mradi huu umeghariwa na Serikali kwa asilimia 100 na gharama ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ni shilingi Bilioni 158 ambao utekelezaji wake umefikia asilimia 99.5. Pia gharama ya ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Chalinze ni shilingi Bilioni 128 ambao utekelezaji wake umefikia asilimia 93.7" amesema Kapinga.

Pia, Meneja wa mradi wa kituo cha kupoza umeme cha Chalinze Mha.Newton Livingstone Mwakifwamba amesema kukamilika kwa mradi wa kituo hicho utasaidia kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme na kuimarisha miundombinu wezeshi ya kupokea Umeme na kuingiza kwenye Gridi ya Taifa.