Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

​MGODI WA GGM WAANZA KUTUMIA U...

​MGODI WA GGM WAANZA KUTUMIA UMEME WA GRIDI BADALA YA MAFUTA

MGODI WA GGM WAANZA KUTUMIA UMEME WA GRIDI BADALA YA MAFUTA

Dkt.Biteko azindua kituo cha kupoza umeme cha GGM (MW 34)

Asema kitaongeza mapato ya Serikali

Aipongeza GGM kuzipa kipaumbele kampuni za kizawa

TANESCO kuingiza mapato ya sh.Bilioni 2 hadi 3 kwa mwezi

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko
amezindua kituo cha kupokea na kupoza umeme katika Mgodi wa Dhahabu wa
Geita (GGM) chenye uwezo wa megawati 34 ambacho sasa kinawezesha GGML
kuanza kutumia umeme wa gridi kwa matumizi yake badala ya mafuta na
hivyo kupunguza gharama za uendeshaji.

Baada ya kuzindua kituo hicho tarehe 13 Agosti 2024 wilayani Geita
mkoani Geita, Dkt.Biteko amesema ujenzi wa kituo hicho ni alama
halisi ya umoja na ushirikiano uliopo kati ya Serikali na Sekta
Binafsi kwani mradi huo umehusisha ujenzi wa laini ya umeme ya kV 33
ambayo imejengwa na TANESCO kwa gharama ya shilingi bilioni 8.04 huku
GGML ikijenga kituo cha kupoza umeme kwa gharama ya Dola za Marekani
milioni 24.

Amesema GGM ilikuwa inatumia shilingi bilioni 130 kwa mwezi kama
gharama za uendeshaji na kwenye umeme wa mafuta ilikuwa inatumia
shilingi bilioni 13.4 kila mwezi na kuathiri mapato yake kwa Serikali,
hivyo kuanza kazi kwa kituo hicho kunapunguza gharama za uendeshaji
kwa mgodi na kupelekea Serikali kuongeza mapato yake, kuongeza ajira
na pia GGM kuweza kutanua shughuli zake.

Dkt.Biteko ameipongeza kampuni hiyo kwa kuanza kutumia umeme wa gridi
ambao unapunguza gharama za uendeshaji ambapo ametoa angalizo kuwa,
kupungua kwa gharama hizo kuguse pia watumishi kwa kuboresha maslahi
yao.

Ameeleza kuwa, umeme mwingi unaozalishwa kwa sasa unatoa uhakika wa
kwenda kwa wananchi na walaji wakubwa kama GGM na kuweka mkazo kuwa,
hayo ni matokeo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuijali sekta
binafsi.

Vilevile, ameipongeza GGM kwa kuzipa kipaumbele kampuni za kizawa
katika kutoa huduma kwenye mgodi huo na kusisitiza kuwa huo ndio
msimamo wa Serikali ya Tanzania wa kuhakikisha kampuni za ndani
zinapewa kipaumbele kwenye miradi mbalimbali.

Dkt. Biteko amewaagiza Watendaji wa Wizara ya Nishati, TANESCO na
Taasisi nyingine za Serikali kujali sekta binafsi kutokana na manufaa
yake ikiwemo kuwa walipakodi wakubwa na kuongeza ajira nchini.

Pia, amewashukuru watangulizi wake katika Sekta ya Nishati, Dkt.
Medard Kalemani na January Makamba ambao katika kipindi chao
wakihudumu kama Mawaziri wa Nishati waliusimamia mradi huo ipasavyo.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amesema
hali ya umeme nchini kwa ujumla ni nzuri huku uzalishaji ukikidhi
mahitaji na ziada kidogo.

Kuhusu usambazaji umeme mkoani Geita amesema kuwa Mkoa una Vijiji 486
na kati ya hivyo vijiji 483 vina umeme sawa na asilimia 99.38.

Ameongeza kuwa, kazi ya kupeleka umeme vitongojini mkoani Geita
inaendelea ambapo kati ya vitongoji 2,197, vitongoji takriban 1000
tayari vina umeme.

Ameongeza kuwa, Mkoa wa Geita umetengewa Shilingi bilioni 8.5 kwa
ajili ya kupeleka umeme maeneo ya migodi na viwanda na utekelezaji
umefikia asilimia 41.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigella amemshukuru
Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira mazuri ya
uwekezaji nchini ambayo yamepelekea wawekezaji kufanya kazi na kuletea
nchi faida akitolea mfano kuwa, katika kipindi cha miaka mitatu GGM
imezalisha tani 51 za dhahabu ambayo ni mafanikio makubwa
yanayochangia ukuaji wa pato la Taifa.

Amemshukuru Rais Samia kwa kuwezesha umeme kufika pia kwenye migodi
ya Wachimbaji wadogo ambapo katika kipindi cha miaka mitatu wachimbaji
wadogo 19 wamepelekewa umeme kwenye migodi yao na kuwezesha uzalishaji
wa kilo za dhahabu takriban 11,000.

Wabunge mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo wamempongeza Rais Samia
pamoja na uongozi wa Wizara ya Nishati kwa kutekeleza mradi huo ambao
una umuhimu mkubwa kwa uchumi wa nchi na mgodi wenyewe.

Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mha.Abubakari Issa
amesema kuzinduliwa kwa kituo hicho kutaiwezesha GGML kuanza kutumia
umeme wa gridi kwenye matumizi yake pamoja na kuongeza mapato ya
TANESCO ambapo inategemewa yataongezeka kwa kiasi cha shilingi bilioni
2 hadi 3 kwa mwezi.



Makamu wa Rais wa kampuni ya Anglo Gold Ashanti-Tanzania
anayeshughulikia Miradi Endelevu, Simon Shayo ameishukuru Serikali
kwa kuweka mazingira mazuri ya biashara na miundombinu madhubuti ya
umeme inayowawezesha kufanya biashara kwa ufanisi.

Amesema mradi huo ni muhimu kwa GGM kwani unawawezesha kupata umeme wa
gridi na kupunguza matumizi ya umeme wa mafuta ambapo gharama
zitapungua kwa asilimia 92.

Viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo ni Wenyeviti na Makamu
Wenyeviti wa Kamati mbalimbali za Bunge, Wabunge kutoka Mkoa wa Geita,
Watendaji kutoka Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (
TANESCO) na GGM.