Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

MHE.KAPINGA AZINDUA JUKWAA LA...

MHE.KAPINGA AZINDUA JUKWAA LA UZIDUAJI 2023

Asema vyanzo vya umeme hasa Sekta ya Gesi ina uhusiano wa moja kwa moja na Sekta ya Uziduaji

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga asema kuwa vyanzo vya kuzalisha umeme vina uhusiano wa moja kwa moja na Sekta ya Uziduaji hususan kwenye Sekta ya Gesi ambayo kwa sasa ina mchango mkubwa katika kuzalisha umeme nchini.

Mhe. Kapinga ameyasema hayo kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko, wakati akizindua Jukwaa la Uziduaji kwa mwaka 2023, lililoandaliwa na Asasi ya kiraia ya HakiRasilimali, tarehe 9 Novemba, 2023 Jijini Dodoma.

Amesema Wizara ya Nishati imekuwa ikishirikiana moja kwa moja na Asasi za Kiraia ikiwemo ya HakiRasilimali inayohusiana na Sekta ya Uziduaji mahsusi katika Sekta ya Gesi.

Amesema majukwaa kama hayo yanawezesha kubadilishana Mawazo ambayo yanaisaidia Serikali kuweza kuboresha mipango yake ili kuwanufaisha zaidi Watanzania kupitia rasilimali zilizopo ikiwemo Gesi.

“Kwa sasa tunatumia kiasi kikubwa cha gesi katika kuzalisha umeme na hivi karibuni tumeendelea kuboresha vyanzo vyetu vya Gesi Asilia ikiwemo Visima vilivyopo Mnazi Bay, Songosongo pamoja na Madimba ili kuweza kuzalisha Gesi Asilia kwa kiasi kikubwa kuweza kuzalisha umeme ili tuondokane na changamoto ya upatikanaji wa umeme nchini”, alisisitiza Mhe. Kapinga.

Vilevile amewapongeza HakiRasilimali kwa mkutano huo uliowakutanisha wadau mbalimbali ili kubadilishana mawazo kuhusu namna ya kutumia rasilimali zilizopo kwa maendeleo pamoja na utunzaji wa mazingira ikizingatiwa kuwa Dunia nzima kwa sasa inapitia changamoto ya Mabadiliko ya Tabianchi.

Jukwaa hilo linatumika kujadiliana na kubadilishana mawazo na kuona namna bora ya kuweza kusonga mbele zaidi kwenye vyanzo vya umeme tulivyonanyo nchini ambavyo ni rafiki na vinalinda mazingira.

Pia kujadiliana kuhusu vyanzo ambavyo vinapatikana nchini lakini vina changamoto mbalimbali ikiwemo mikataba ya kimataifa inayozuia matumizi yake, hivyo jukwaa hilo litaona namna bora ya kukubaliana na mikataba hiyo ili kuwawezesha Watanzania kunufaika na matumizi ya rasilimali zilizopo katika kuzalisha umeme.

Alimalizia kwa kusema kuwa Serikali imekuwa ikithamini sana mchango wa Asasi za Kiraia kwenye masuala yanayohusu maendeleo ya Watanzania.