Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. K...

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Kapinga akutana na Uongozi wa TANESCO

# Awataka kutatua changamoto Sugu zinazowakabili wananchi.

# Asema Viongozi wa Chama na Serikali washirikishwe katika miradi iliyo katika maeneo yao.

Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga amekutana na Uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na kuwaeleza kuwa wahakikishe wanamaliza changamoto sugu zinazowakabili wananchi.

Mhe. Judith amekutana na Uongozi huo tarehe 2 Novemba, 2023 Jijini Dodoma kwa lengo la kuzungumza nao na kufahamu namna walivyojipanga katika katika kutatua changamoto moto mbalimbali za umeme kwa wananchi.

Katika Mazungumzo yake, Mhe. Kapinga ameuelekeza Uongozi huo kuwahakikisha wanatatua changamoto sugu kwa kufanya kazi za ziada ili kuweza kupata mabadiliko katika utoaji wa huduma.

Amewataka kuweka mipango ya muda mrefu ili kumaliza changamoto ndogondogo ikitolea mfano kukatika kwa umeme.

Pia amewataka kutatua kero zinazowakabili wananchi kwa wakati na kuzitolea ufafanuzi.

“Dunia imeendelea sana na teknolojia imekuwa mno, umeme kwa sasa si anasa hivyo kila mtu anahitaji huduma hiyo kwa matumizi ya aina mbalimbali, tuhakikishe tunawafikia wananchi ili waendane kulingana na Dunia ya sasa”, alisisitiza Mhe. Kapinga.

Kuongeza kasi ya kuunganisha wateja wapya na kuyafikishia huduma ya umeme maeneo ambayo bado hayajafikiwa na huduma hiyo.

Pia amewataka kuwashirikisha na kuwafahamisha viongozi wa Chama na Serikali wakiwemo Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Watendaji wa Serikali za Mitaa kuhusu miradi mbalimbali inayoendelea katika maeneo yao ili wafahamu vema na kuwaeleza wananchi wanaowaongoza.

Pamoja na mambo mengine amewataka kusimamia kwa ukaribu miradi ya vipaumbele ikiwemo ule wa kupelekea umeme Katavi, Rukwa, Kigoma, Kagera, Mtwara na Lindi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Gissima Nyamohanga, amemueleza Naibu Waziri kuwa wamepokea maelekezo hayo na wapo tayari kwa utekelezaji.

Mkutano huo pia umehudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Athumani Mbuttuka, Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Innocent Luoga,na Viongozi wengine waandamizi kutoka TANESCO.