TPDC YAHIMIZA WANANCHI KULINDA MIUNDOMBINU YA BOMBA LA GESI ASILIA.
Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeendelea kuwashirikisha wananchi katika kulinda miundombinu ya bomba la gesi asilia, likieleza kuwa usalama wa miundombinu hiyo unategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano wa jamii nzima.
Katika kuimarisha ulinzi huo, TPDC inaendelea kutekeleza mpango wa utoaji elimu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia mkoani Pwani, hususan katika Wilaya za Rufiji, Kibiti na Mkuranga.
Lengo la mpango huo ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu hiyo pamoja na kuwajengea uwezo wa kutambua na kuripoti mapema vitendo au shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wake.
Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bi. Ashura Hoja alisema “Bomba la gesi asilia ni rasilimali ya taifa hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kuwa mlinzi wa miundombinu hii na kutoa taarifa mapema mnapoona shughuli zisizo za kawaida karibu na bomba la gesi”. Alisema Bi. Hoja
Aidha, TPDC imewapongeza wananchi wa maeneo husika kwa mwitikio wao katika kushiriki kulinda miundombinu hiyo, huku ikiwataka kuendelea kuwa makini zaidi kwani uharibifu wowote unaweza kuathiri huduma muhimu pamoja na maendeleo ya taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, mwananchi wa Kijiji cha Jaribu Mpakani, Wilaya ya Kibiti, Bw. Kassimu Iddi alisema elimu inayotolewa na TPDC imeleta mabadiliko makubwa ya mtazamo kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda bomba la gesi.
“Sasa tunaelewa kuwa kulinda bomba la gesi ni kulinda maisha yetu na maendeleo ya taifa letu. Tumeamua kuwa walinzi wa kwanza wa miundombinu hii”. Alisema Kassimu
TPDC imeendelea kutoa wito kwa jamii zote zinazoishi karibu na bomba la gesi asilia kushiriki kikamilifu katika mfumo wa ulinzi wa pamoja, ili kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.