Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

​WATANZANIA WATAKIWA KUTUMIA F...

​WATANZANIA WATAKIWA KUTUMIA FURSA ZA UJENZI BOMBA LA MAFUTA

WATANZANIA WATAKIWA KUTUMIA FURSA ZA UJENZI BOMBA LA MAFUTA

Hafsa Omar-Kagera

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewataka Wananchi watakaopitiwa na ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) kujitokeza na kuzitumia fursa mbalimbali ambazo zitapatikana wakati wa ujenzi wa bomba hilo.

Ameyasema hayo, Julai 17, 2021 wakati wa Mkutano na wadau mbalimbali kujadili fursa za Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta, uliofanyika katika Wilaya ya Misenyi, Mkoani Kagera.

Dkt. Kalemani amezitaja fursa hizo,ambazo ni ujenzi wa viwanda mbalimbali vitakavyozalisha bidhaa ambazo zitatumika katika ujenzi wa mradi.

Pia, amesema Watanzania zaidi ya 15,000 watajiriwa katika kipindi cha ujenzi wa bomba hilo, na kuwataka pia kuchangamkia fursa ya kufanya biashara mbalimbali ambazo zitawaingizia kipato.

Amesema, lengo la Mkutano huo ni kujenga uelewa na kuwaeleza wananchiwajibu wao ili waweze kushiriki katika shughuli mbalimbali wakati wa ujenzi husika, ambapo ameeleza kuwa zaidi ya asilimia 80 kazi za mradi huo zitafanywa na Watanzania.

“Mradi huo wakati wa ujenzi utaoa fursa kwa Watanzania wengi tunawaomba Watanzania kuchukua nafasi hii kuwekeza katika sekta mbalimbali, na kwa wale ambao hawana mtaji tunaongea na mabenki ili waweze kuwakopesha mikopo ya masharti nafuu ”alisema.

Aidha, amesema utekelezaji wa mradi umeanza na upo kwenye hatua za mwisho za ulipaji wa fidia, na baadhi ya maeneo tayari ujenzi wa barabara za kuelekea kwenye mradi umeanza.

Ameongeza kuwa, ujenzi wa mradi huo utachukua takribani miaka mitatu na utagharimu dola za kimarekani bilioni 3.5.

Waziri Kalemani, pia ameeleza manufaa ya mradi huo kwa kufafanua kuwa katika Mikoa ya Singida, Tabora na Simiyu, maeneo hayo ambayo bomba linapita yanatarajiwa nayo kutoa mafuta ambapo amesema nchi itatumia bomba hilo kupitisha mafuta hayo.

Pia, amewataka wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Serikali pamoja na wawekezaji na kushiriki katika ulinzi wa bomba hilo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Charles Mbuge amesema, ujenzi wa mradi huo utainua uchumi wa Mkoa wa Kagera na kwa nchi kiujumla.

Vilevile, amesema atahakikisha mradi utajengwa na kusimamiwa kwa umakini, na mataifa mengine yatajua kuwa Watanzania ni watu makini na wazalendo na hilo litasadia nchi kuendelea kupata fursa mbalimbali za miradi kutoka kwenye mataifa ya jirani.

Pia, amesema kuwa uongozi wa Mkoa huo utahakikisha mradi huo unalindwa na utakuwa kuwa salama mda wote wa ujenzi na hata ukikamilika.

Naye, Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kuchukua fursa mbalimbali ambazo zitakazopatikana kwenye ujenzi wa mradi na kuwataka kujivunia ujenzi huo kwani unaenda kuwasaidia kujikwamua kiuchumi.