Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

​Waziri wa Nishati azindua mat...

​Waziri wa Nishati azindua matumizi ya Gesi Asilia katika nyumba 300 Mtwara

Waziri wa Nishati azindua matumizi ya Gesi Asilia katika nyumba 300 Mtwara

Na Teresia Mhagama,

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amezindua matumizi ya Gesi Asilia majumbani katika nyumba 300 ambazo zimeunganishwa na nishati hiyo wilayani Mtwara kwa gharama ya shilingi milioni 961.7

Uzinduzi huo ulifanyika tarehe 25 Agosti, 2021 katika Mtaa wa Kyangu wilayani Mtwara, na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato, Viongozi mbalimbali katika Mkoa wa Mtwara wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Dunstan Kyobya, Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Adam Zuberi, Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Khalfan Khalfan, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt.James Mataragio na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Mhandisi Godfrey Chibulunje.

“ Hii ni awamu ya Pili ya usambazaji Gesi Asilia majumbani katika Mkoa wa Mtwara kwani katika awamu ya kwanza wateja takriban 125 waliunganishwa na wananufaika na gesi hii katika mitaa ya Reli A na B, Kyangu, Masandube na Lilungu.” Alisema Dkt.Kalemani

Ili kuhakikisha nishati hiyo inawafikia wananchi wengi zaidi, aliiagiza TPDC na kampuni yake tanzu inayohusika na usambazaji wa Gesi Asilia (GASCO), kusambaza gesi hiyo kwa wananchi wote bila kubagua kutokana na manufaa yake mbalimbali kama vile unafuu wa gharama kulinganisha na nishati nyingine zinazotumika kupikia, pia inapunguza uharibifu wa mazingira.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya Gesi Asilia mkoani humo yasiishie tu kwenye Taasisi na majumbani, hivyo ameiagiza TPDC kufungua kituo cha kujazia gesi kwenye magari na kwenye viwanda mbalimbali.

Vilevile, Waziri wa Nishati aliiagiza TPDC, kuendelea kutumia vifaa vinavyotengenezwa ndani ya nchi katika shughuliza usambazaji Gesi Asilia majumbani na kueleza kwa kufanya hivyo kutaleta manufaa mbalimbali ikiwemo kuongezeka kwa ajira na uhakika wa upatikanaji wa vifaa.

Aliongeza kuwa lengo la Serikali sasa ni kupeleka Gesi Asilia hadi vijijini kupitia mpango wa usambazaji nishati vijijini, hivyo aliwaagiza TPDC kuendelea kuwahamasisha wananchi kutumia nishati hiyo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato, alieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita itahakikisha kwa Gesi Asilia iliyopo inawanufaisha wananchi mkoani Mtwara na watanzania kwa ujumla.

Kuhusu maagizo mbalimbali yaliyotolewa na Waziri wa Nishati, alieleza kuwa atahakikisha yanatekelezwa kwa ufanisi kwa kushirikiana na Taasisi zilizo chini ya Wizara zinazohusika na nishati hiyo.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, James Mataragio alisema kuwa kazi ya usambazaji Gesi Asilia majumbani ni endelevu kwani katika mwaka 2021/22 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuunganisha nishati hiyo katika nyumba nyingine 300.

Kuhusu mradi wa usambazaji Gesi Asilia majumbani wa Awamu ya Pili, alieleza kuwa umetekelezwa na wataalam wa ndani ambao ni wahandisi watanzania kutoka kampuni ya GASCO tofauti na mradi wa Awamu ya kwanza ambao ulitumia wakandarasi na hivyo gharama zake zilikuwa juu tofauti na mradi wa Awamu ya Pili.

Alifafanua kuwa, mradi wa Awamu ya Kwanza ulitumia katribani shilingi Bilioni 3.2 huku mradi wa Awamu ya Pili ukitumia shilingi milioni 961.7 hivyo Serikali imeokoa fedha takriban shilingi Bilioni 2.

Alisema kuwa, Mji wa Mtwara ni mojawapo ya miji ambayo kwa sasa inanufaika na matumizi ya Gesi Asilia kwani mji huo umeunganishwa na miundombinu yenye jumla ya km 56.7 inayopeleka gesi kwa matumizi ya kuzalisha umeme, wateja wa majumbani, Taasisi na kiwanda cha Dangote.