Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Ministry of Energy

DKT.BITEKO ASHUHUDIA UTIAJI SA...

DKT.BITEKO ASHUHUDIA UTIAJI SAINI MIKATABA MIWILI YA KIHISTORIA YA GESI ASILIA

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko leo

ameshuhudia uwekaji saini Mkataba wa Mauziano ya Gesi Asilia
itakayozalishwa katika eneo la Ntorya Kitalu cha Ruvuma kilichopo
mkoani Mtwara na uwekaji saini hati ya Makubaliano kwa ajili ya
kuanzisha mahusiano ya kujenga miundombinu ya kusambaza Gesi Asilia
kwa teknolojia ya miundombinu midogo ya kubadilisha Gesi Asilia kuwa
Kimiminika (Mini-LNG).

Hafla ya utiaji saini imefanyika tarehe 10 Januari, 2024, Wilaya ya
Magharibi A, Mkoa wa Mjini Magharibi ambapo Mkataba wa Mauziano ya
Gesi Asilia itakayozalishwa eneo la Ntorya umesainiwa kati ya Shirika
la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kampuni ya ARA Petroleum ya
Oman na Ndovu Resources ya Uingereza.Hati ya Makubaliano kwa ajili ya
kuanzisha mahusiano ya kujenga miundombinu ya Gesi Asilia imesainiwa
kati ya TPDC na Kampuni ya KS Energy.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Biteko amesema kuwa, Mkakati wa
Wizara ya Nishati ni kuhakikisha kuwa inasimamia ipasavyo Sera ya
Nishati ya mwaka 2015 na kuhakikisha kuwa kunakuwa na upatikanaji wa
nishati safi ambayo itawafikia wateja mbalimbali kwa urahisi na bei
nafuu.

Amesema kuwa, lengo la nchi ni kuwa na nishati inayotokana na vyanzo
mbalimbali ikiwemo Jua, Upepo, Gesi na Maji ili Gesi Asilia iliyopo
itumike pia kwa kiasi kikubwa kwenye maeneo mengine kama viwanda na
majumbani badala ya kutumika kwa kiasi kikubwa kwenye umeme na pia
kupunguza matumizi ya mafuta.

“Mkakati wetu ni kubadilisha suala hili la Gesi Asilia kutumika zaidi
kwenye umeme ambayo ni takriban asilimia 80, tunataka kuwe na nishati
mchanganyiko nchini ili gesi itumike kwenye viwanda na majumbani na
pia tupunguze utegemezi wa mafuta.” Amesema Dkt. Biteko

Ameongeza kuwa, TPDC sasa wana mkakati utakaowezesha kuwa na mgawanyo
wa matumizi ya Gesi Asilia ambapo matumizi kwenye umeme itakuwa
asilimia 38, majumbani na viwandani itakuwa asilimia 32 na asilimia 10
itabaki majumbani tofauti na ilivyo sasa ambapo matumizi ya Gesi
viwandani na majumbani ni asilimia 28 na asilimia iliyobaki kwa kiasi
kikubwa inaenda kwenye umeme.

Kuhusu hati iliyosaniwa ya miundombinu midogo ya LNG, Dkt. Biteko
amesema kuwa, nchi ina kilometa za mraba 945,000 na kwamba pamoja na
uwepo wa Bomba la Gesi Asilia nchini njia rahisi ya kufanya Gesi
iwafikie watu wengi ni kuigeuza gesi kuwa kimiminika na kusafirisha
kwa magari kwenda kwenye maeneo ambayo watu watatumia hivyo kutiwa
saini kwa makubaliano hayo kutawezesha Gesi kuwafikiwa wananchi wengi
zaidi.

Amesema kuwa, Serikali iko tayari kushirikiana na wawekezaji hao ili
kuwafikishia wananchi nishati ya uhakika kutoka vyanzo mbalimbali huku
akitolea mfano utekelezaji wa mradi wa megawati 50 unaotokana na Jua
wilayani Kishapu, Mkoa wa Shinyanga na ujenzi wa miradi mingine ya
uzalishaji, usafirishaji na usambazaji umeme.

Ameeleza kuwa, Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan anafuatilia kwa karibu
utekelezaji wa miradi ya nishati nchini kwani anachotaka ni watu
wapate umeme wa uhakika pamoja na nishati nyinginezo.

Vilevile amesema kuwa, Serikali haitaki urasimu katika utekelezaji wa
mipango inayojiwekea kwani nia ni kwenda na wakati na kufanya vitu
vitokee kwa manufaa ya kizazi cha sasa na cha badaye.

Amesema kuwa Serikali inaangalia vitu muhimu ambavyo vitaondoa watu
kwenye umaskini kwa haraka zaidi ikiwemo uwepo wa miundombinu ya
barabara, anga, reli, Bandari na uwepo wa nishati ya uhakika ambapo
kwa upande wa Wizara ya Nishati, zinafanyika kila jitihada ili kuwe na
nishati ya kutosha na ya uhakika.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Ahmed Abbas Ahmed
amesema kuwa, mradi miradi hiyo ina umuhimu mkubwa ikiwemo katika
mikoa ambapo rasilimali hiyo inazalishwa na kwamba watahakikisha
wanaisimamia kwa ajili ya maendeleo ya Mtwara na nchi kwa ujumla.

Amemshukuru, Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa miradi
mbalimbali ya kimkakati mkoani Mtwara ikiwemo ya utafutaji na
uzalishaji wa Gesi Asilia.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame alisema kuwa, Mkataba
wa mauziano ya Gesi Asilia uliosainiwa leo utawezesha kuongeza gesi
iliyogunduliwa nchini ambapo mradi huo unategemea kuzalisha kiasi cha
kuanzia futi za ujazo milioni 60 kwa siku hadi kufikia futi za ujazo
milioni 140 kwa siku katika kipindi cha miaka 3.

Ameongeza kuwa, kukamilika kwa mkataba huu kutawezesha shughuli
nyingine za uendelezaji kufanyika kama vile, ujenzi wa miundombinu ya
kukusanya gesi kutoka visimani, ujenzi wa miundombinu ya kukusanya
gesi kutoka visimani, ujenzi wa miundombinu ya usafishaji wa awali
ikiwemo kutoa maji na ujenzi wa bomba la kilometa 34 la kusafirisha
gesi asilia hadi kiwanda cha kuchakata gesi kilichopo Msimbati,
Madimba mkoani Mtwara.

Ameeleza kuwa, katika kitalu cha Ruvuma Gesi iliyogunduliwa na
kuhakikiwa ni futi za ujazo bilioni 1.6.

Kuhusu Hati ya Makubaliano kwa ajili ya utekelezaji wa ujenzi wa
miundombinu midogo ya kubadilisha Gesi Asilia kuwa kimiminika
(Mini-LNG), ameeleza kuwa, mradi utakuwa wa kwanza kufanyika nchini na
utawezesha kupunguza kiu ya watanzania kutumia Gesi Asilia hata kwa
maeneo yaliyo mbali na miundombinu ya mabomba na hivyo kuchochea
matumizi ya nishati safi nchini.