SHIMIWI 2026; WACHEZAJI NISHATI WASISITIZWA NIDHAMU, UZALENDO NA USHINDI
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Bw. Petro Lyatuu, amewataka watumishi watakaoiwakilisha Wizara katika Michezo ya SHIMIWI 2026 kuonesha nidhamu, uzalendo, mshikamano na ari ya ushindi, huku wakidumisha heshima ya Wizara na Serikali kwa ujumla.
Wito huo ameutoa wakati akizungumza na timu ya Wizara inayotarajiwa kushiriki mashindano hayo yatakayofanyika mkoani Kilimanjaro kuanzia Septemba 20 hadi Oktoba 7, 2026.
Bw. Lyatuu amesema Wizara ina imani kubwa na timu hiyo kutokana na maandalizi yaliyofanyika kwa kipindi cha takribani mwezi mmoja, akibainisha kuwa ushiriki katika SHIMIWI ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Michezo inayolenga kuimarisha afya, mshikamano na mahusiano miongoni mwa watumishi wa umma.
“Ninyi ni mabalozi wa Wizara ya Nishati, tunatarajia kuona nidhamu, kujituma, ushirikiano na uwajibikaji katika mashindano haya, mlinde taswira ya Wizara na Serikali kwa kuwa mfano bora huku mkizingatia maadili ya Utumishi wa Umma,” amesema Bw. Lyatuu.
Aidha, amewahimiza wachezaji kuzingatia sheria na taratibu za mashindano, kuwa na moyo wa kujiamini na kufanya kazi kwa umoja ili kufikia malengo kwa kuona timu zikifanya vizuri zaidi kuliko miaka iliyopita na kurejea na matokeo yatakayoiwezesha kujivunia ushiriki wake.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bi. Ziana Mlawa, amesema jumla ya watumishi 36 kutoka Wizara na taasisi zake watashiriki michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, netiboli, riadha, kuvuta kamba, darts, bao na karata.
Bi. Mlawa amesisitiza kuwa lengo la Wizara mwaka huu ni kwenda kushindana kwa kiwango cha juu na kupata matokeo bora, sambamba na washiriki kutumia mashindano hayo kujenga mahusiano ya kikazi, kubadilishana uzoefu na kujifunza kutoka kwa watumishi wa Wizara nyingine.
Akizungumza kwa niaba ya timu, Kocha Damian Chonya ameushukuru uongozi wa Wizara kwa hamasa na maandalizi yaliyowezesha timu kuwa tayari kwa mashindano hayo.
Amesema wachezaji wamejiandaa vyema kimwili, kiufundi na kinidhamu, huku wakiahidi kuitumikia Wizara kwa juhudi na kujituma ili kufikia matokeo yanayotarajiwa katika SHIMIWI 2026